Ads 468x60px

Mar 10, 2025

RAMADHAN KAREEM - PT 3 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo na mnaendelea na ibada za Mwezi Mtukufu. Tunaendelea na risala yetu. 

 

 

 Baada ya Kumshukuru Allah na kumtakia Rehma Mtume Muhammad , hapo juu ni aya ya 10 na 11 ya Sura As-Swaaf kutoka Quran inayozungumzia jihad na ndiyo itakuwa mada yetu.

 

Tunaendelea na mwezi Mtukufu wa Ramadhani, mwezi ambamo mambo kadhaa yamedhihirika. Ni katika mwezi huu saumu ikafaradhishwa, qiyam ya usiku yaani sala ya tarawih ikawekwa ni jambo la thawabu, ni mwezi wa kuomba dua na ni mwezi ambamo dua inakubalika. Pia ni mwezi ambamo mna usiku wa Lailatul Qadri. Fadhila nyingine ni kuwa Quran imetelemshwa katika mwezi huu.

Wafasiri na wanazuoni wakuu wanaelezea kuwa vitabu vyote vya mbinguni vimeteleshwa katika mwezi huu.

 

Ni katika mwezi huu katika maeneo ya Badri, vita kati ya Waislamu na makafiri, iitwayo vita vya Badri, ilitokea ambayo ilidhihirisha ujasiri wa Uislamu. Makafiri walidhalilika mno na hawakutegemea kabisa. Hivyo leo tutazungumzia kuhusu vita vya Badri ili kujipatia thawabu za kuwakumbuka Masahaba mashujaa waliojitolea kwa hali na mali kuitetea Uislamu.

 

Tafsiri ya aya: Enyi mloamini, je Nisiwaonyeshe biashara itakayowaokoa na adhabu kali? Muaminini Allah na Mtume Wake, na piganeni jihad katika njia ya Allah, kwa mali yenu na nafsi zenu, haya ni bora kwenu ikiwa mnafahamu. (SURA: AS-SWAFF: 10-11)

 

Biashara ni jambo ambalo inampatia mtu faida. Hapa Allah Anazungumzia kuleta imani juu ya Allah na Mtume Wake, kusoma kalima, ndipo itamletea mtu faida; vinginevyo hatapata faida yoyote. Kisha Allah akaagiza jihad katika njia Yake kwa mali na nafsi zetu; na hii akaitaja kuwa ni bora kwetu.

 

Hivi sasa Waisalmu wanadhalilika ulimwenguni ni kwa sababu ya kuacha jihad. Pili mali na pesa imewafanya watu kuwa waoga. Tatu jihad huzidisha hadhi ya Uislamu. Uislamu ni dini ya amani, lakini pindi inapoandamwa kutaka kuangamizwa, basi ni vyema ikahifadhiwa kwa jihad. Anaeuawa katika jihad ni shahidi. Pia anaejeruhiwa katika jihad, basi siku ya kiyama damu itatoa ushahidi wa kunukia kama zafarani. Shahidi hataogeshwa bali atakafiniwa katika nguo zenye damu, atasaliwa jeneza na kuzikwa. Siku ya kiyama atafufuliwa na nguo zake za damu.

 

Hadithi: Mtume amesema kuwa mtu mwenye macho aina mbili hataingia motoni. Moja: ni mwenye kutokwa na machozi katika hofu ya Allah na PILI macho yaliyokesha wakati wa jihadi ikichunga uvamizi wa adui.

Hadithi: Mtu huyu hataingia motoni ambae miguu yake ikapatwa na vumbi katika njia ya Allah.

 

 

Katika vita vya Badri, Waislamu walikuwa 313 tu wakiwa na farasi 17 tu na mikuki kama 8 na pia hawakujianadaa kabisa kupigana. Makafiri walikuwa kati ya 900 na 1,000 na kila mmoja alikuwa na farasi au ngamia na vifaa vyote na walijiandaa kikamilifu. Makafiri walikuja na dhamira ya kuwadhalilisha Waislamu. Masahaba walimtayarishia Mtume banda la kukaa na kutoa amri. Iliponadiwa nani atakaemlinda Mtume , AbuBakr Siddiq ndiye aliyejitokeza.

 

Makafiri 70 waliuawa katika vita wakati Masahaba 14 tu wakawa mashahidi. Usiku wa kuamkia siku ya vita, Mtume alipotembelea uwanja wa vita, aliweka alama kuwa kafiri Fulani atakufa hapa na Fulani hapa, na ndivyo ikawa.

 

Wakati wa vita, walikuja watoto wawili kwa AbdulRahman bin Auf na kumwambia waonyeshwe aliko Abu Jahal ili wakamuue kwani anamtukana sana Mtume . Walipoonyeshwa, mmoja alimpiga panga la nguvu hadi mguu kuvunjika. Jeuri lake likawa pale tu kwani kabla ya kufa alisikitika mno kupigwa na watoto wadogo badala ya jemedari kama yeye.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa.

 

JazakAllah.

Mar 4, 2025

RAMADHAN KAREEM - PT 2 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo na mnaendelea na ibada za Mwezi Mtukufu. Tunaendelea na risala yetu.

Baada ya Kumshukuru Allah na kumtakia Rehma Mtume Muhammad , imesomwa aya ya Quran inayozungumzia saumu na ndiyo itakuwa mada yetu.

 

Tafsiri ya aya:

Enyi mloamini mmefaradhishiwa kufunga kama walivyofaradhishiwa wale walikutangulieni, ili mpate kumcha Mwenyezi Mungu.

Hadithi tuliyosimulia Ijumaa iliyopita, ina maelezo zaidi, na tutazichambua kwa ufupi.

 

Tumefaradhishiwa saumu. Ila kama kuna mgonjwa au msafiri au mwanamke katika siku za hedhi zake, hao wameruhusiwa kutofunga siku hizo. Baada ya kukamilisha idadi ya 29 au 30, basi wanatakiwa wafunge siku walizoacha. Ila hawaruhusiwi kula hadharani. Pia mtu mzee asiye na nguvu na wala hatarajii kupona, itambidi atoe fidia badala ya saumu zake. Lau kama atapata nguvu, basi ni bora kwake kufunga na si kutoa fidia.

 

Qiyam / ibada ya usiku imefanywa kuwa ni ya thawabu. Ibada ya usiku ni raka 20 za Tarawih, nayo ni Sunnah iliyosisitizwa kwa wanaume na wanawake. Ni bora kwa kina mama kusali nyumbani. Hadi mwanzoni mwa Ukhalifa wa Sayyidina Umar, Masahaba walisali Tarawih peke yao. Ndipo Sayyidina Umar aliwakusanya nyuma ya imam mmoja nae ni Ubay bin Ka'ab, ambae aliwasalisha rakaa 20. Baadhi ya watu wanadai Tarawih ni raka 8. Ikumbukwe raka 8 ni tahajjud na si Tarawih.

Pia kiakili naomba tuzingatie; ikiwa Tarawih ni rakaa 8 na sisi tunasali rakaa 20, siku ya Kiyama Allah Akituuliza kwa nini umezidisha rakaa 12, basi japo tutaweza kumuomba kwa Rehema zake atujaalie thawabu ya ziada kwa hizo rakaa 12. Lakini je wanaosali rakaa 8 na Allah akiwauliza kuwa Tarawih ni 20 kwa nini mkasali 8 tu, hebu jiulize hizo rakaa 12 watazitoa wapi!! Naomba tusipumbazike na wanaodai kuwa eti ni rakaa 8 tu!! Laa hasha! Tarawih ni rakaa 20.

 

Mna usiku mmoja ambayo ibada yake ni bora kuliko ibada ya miezi 1,000. Miezi 1,000 ni miaka 83 na ieleweke kuwa umri wa ummah huu ni karibia miaka 60.

 

Imeelezwa kuwapunguzia mzigo wafanyakazi wenu mwezi huu. Mtume amesema kuwa mwenye kumpunguzia mzigo mfanyakazi wake, basi Allah atampunguzia mzigo siku ya Qiyama.

 

Mtume ameeleza kuwa siku zake 10 za mwanzo Allah anawarehemu waja wake, 10 za kati Allah anawasamehe waja wake na 10 za mwisho ni kuongoka na moto wa jahannam.

Imeelezwa kukithirisha mambo manne: Kalima, istighfar, kuomba Pepo na kuomba huru na moto wa jahannam.

Mwenye kumfuturisha Muislamu mwenzake, hujaaliwa thawabu ya saumu moja mwenye kumnywesha maji, basi Allah atamjaalia maji ya Kauthar na hatashikwa na kiuu hadi kuingia Peponi.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa.

 

JazakAllah.

Feb 27, 2025

AHLAN WA SAHLAN YAA SHAHRI RAMADHAN [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo.

 

Mwezi mtukufu ndiyo umeingiza mguu mmoja kwetu na in sha Allah, tutakuwa ndani ya swaum. Allah Atujaalie wepesi, afya njema na kibwa zaidi Atukubalie ibada zetu, ameen.

 

Ifuatayo ni utangulizi wa risala za mwezi Ramadhan. 

 

Baadhi ya matukio (tarehe) muhimu katika mwezi wa Ramadhani:

Tarehe 1: Kuzaliwa kwa Sheikh Sayyid AbdulQadir Jilani

Tarehe 3: Fatima binti Rasul RadwiyAllahu Anha kuiaga dunia

Tarehe 10: Mama Khadija RadwiyAllahu Anha kuiaga dunia.

Mama aliyekuwa tajiri na mfanyabiashara maarufu wa Makkah, aliolewa na Mtume akiwa na umri wa miaka 40 wakati umri wa Mtume ulikuwa miaka 25. Na ilitokana na uaminifu wa Mtume katika safari zake za biashara ya Mama Khadija. Mtumwa wake alimsimulia kuwa kila Mtume alipotembea basi kuwa wingu nayo ilitembea nae ikimpa kivuli. Na pia katika safari yake ya kwanza tu, wakati wengine walipata hasara katika biashara zao, Mtume alimletea faida maradufu Mama Khadija. Hicho kilimvutia sana hadi kupeleka posa la kutaka kuolewa na Mtume.

Baada ya kuolewa, Mama Khadija alisalimisha mali yake yote kwa Mtume ili itumike katika kuinusuru Uislamu.

 

Tarehe 17: Vita vya Badri (kisa kitafuata katika risala ya baadae) na Mama Aisha RadwiyAllahu Anha kuiaga dunia.

 

Mama Aisha, ambae ni binti wa Sayyidina AbuBakr Siddiq RadwiyAllahu Anhu, alikuwa mjuzi sana katika mambo ya dini na anamfuatia Bwana Abu Huraira katika kupokea riwaya kwa wingi Hadithi kutoka kwa Mtume.

 

Tarehe 21: Kuuawa shahidi kwa Sayyidina Ali RadwiyAllahu Anhu.

 

Usiku wa 21, 23, 25, 27 na 29 ni Laylatul Qadr.

 

Katika 10 za mwanzo, tukithirishe sana kutamka ALLAHUMMAR HAMNA YAA ARHAMAR RAAHIMIN.

 

Katika 10 za kati, tukithirishe sana kutamka ALLAHUMMA RABBANAGH FIRLANA DHUNUBANA YAA RABBAL AALAMIN.

 

Na katika 10 za mwisho: ALLAHUMMA QINA ADHABANNAARI WA-ADKHILNAL JANNATA MA-AL ABRAARI YAA AZIZU YAA GHAFFAAR.

 

RAMADHAN KAREEM!

Feb 8, 2025

NISF SHA'ABAAN [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

Natumai hamjambo.

Katika mwezi huu wa Sha’abaan mna usiku, ambao ni mwezi 14 kuamkia 15, ambamo mahesabu ya binadamu kwa mwaka uliopita hufungwa na vile vile matukio ya mwaka unaokuja huandikwa. Hivyo ni vyema tukawa katika ibada ili daftari letu kwa mwaka unaoisha ufungwe kwa ibada na ule wa mwaka unaoanza nao ufunguliwe kwa ibada.

Mmojawapo ya ibada iliyopendekezwa ni kusoma Sura Yasin mara 3 pamoja na Dua ya Nisf Sha’abaan baada ya sala ya Maghrib.

Pia Saum ya Nisf Sha'baan nayo ina fadhila zake.

Allah Atujaalie wepesi.

Jazak Allah.

Jan 30, 2025

SHA'ABAAN [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo.

 

Mwezi wa nane katika Kalenda ya Kiislamu ni Sha'abaan. Utukufu wa mwezi huo juu ya miezi mingine ni kama ule wa Mtume juu ya Mitume wengine.

 

BAADHI YA TAREHE MUHIMU:

 

Qiblah ilibadilishwa kutoka Baytul Maqdis na kuwa Al Kaaba.

 

Imam Abu Hanifa, mmoja kati ya Maimamu wanne, kuiaga dunia hii tarehe 2.

 

Imam Husein RadwiyAllahu kuzaliwa tarehe 6.

 

Usiku wa kuwa huru na moto wa Jahannam (au kasimatu rizki) tarehe 15.

 

KUBADILIKA KWA QIBLAH:

 

Baytul Maqdis (Msikiti wa Aqsa) ulikuwa ndiyo Qiblah ya mwanzo ya Waislamu. Karibu Mitume wote waluielekea katika sala zao. Mtume alitamani sana kuelekea Al Kaaba tangu mwanzo tu.

 

Kila Mtume aliposali akielekea Baytul Maqdis, Mayahudi hukasirika sana na hata husema "inakuaje Mtume wenu anawaamrisheni kutenda kinyume na Mayahudi na inapokuja swala ya ibada basi anauelekea mji wetu (Jerusalem)?" Mtume hakujisikia kabisa vizuri kwa maneno hayo ya Mayahudi na alitamani sana kuelekea Al Kaabah.

Sub-Hanallah! Mara moja Allah Akatelemsha aya inayoelezea: "Tunashuhudia ukiinua uso wako mara kwa mara mbinguni. Basi tutakuelekeza upande wa Qiblah uiridhiayo wewe. Elekea Msikiti wa Haraam (Al Kaaba) sasa hivi, na enyi Waislamu! Elekeze nyuso zenu huko pia, popote mlipo .." (Quran Tukufu 2:144). Zingatieni watukufu Waislamu kuwa badiliko la Qiblah limetokea kwa sababu tu ya kumridhisha Mtume . Kuanzia hapo qiblah yetu ni Al Kaaba huko Makkah.

 

IMAM ABU HANIFA:

 

Jina lake hasa ni Nooman bin Thabit bin Zuta bin Mah. Alizaliwa katika mji wa Kufa, Iraq, mwaka wa 80 Hijria. Alikuwa katika zama tukufu wa Tabi'in (wale waliowafuata Masahaba).

 

Amepokea Abu Huraira RadwiyAllahu Anhu kuwa Mtume amesema kuwa : Katika ummah wangu atakuja mtu ataitwa Abu Hanifa. Siku ya Qiyama yeye (Abu Hanifa) ndiye atakuwa taa ya ummah wangu. Hadithi nyingine imeeleza kuwa "katika kila karne idadi Fulani ya ummah wangu utakuwa na daraja ya juu; Abu Hanifa atakuwa na daraja ya juu zaidi katika zama zake".

 

Miongoni mwa Masahaba aliokutana nao ni Sayyiduna Anas bin Maalik, Sayyiduna Sahl bin Saad na Sayyiduna Abul Tufail Amir bin Wathila RadwiyAllahu Anhum. Imam Abu Hanifa alipata elimu ya dini kupitia baadhi ya Masahaba na wanazuoni wapatao kama 4,000. Baadhi ya Masahaba ni Sayyiduna Hammad Basri, Sayyiduna Ata bin Abi Rabah, Sayyiduna Ikramah, Sayyiduna Imam Baaqir, Sayyiduna Imam Jafar Saadiq, Sayyiduna Abu Ali, Sayyiduna Abu Hurayrah, Sayyiduna Abdullah Ibn Umar, Sayyiduna Aqabah bin Umar, Sayyiduna Safwaan, Sayiduna Jabir na Sayyiduna Abu Qatadah RadwiyAllahu Anhum.

 

Imam Abu Hanifa alikuwa mfanya biashara na kila Ijumaa alikuwa akitoa sarafu 20 za dhahabu kwa wasiojiweza kama sadaka. Kwa muda wa miaka 40 Imam alisali sala ya Alfajiri kwa udhu ule ule wa sala ya Ishai (kwa maana usiku kucha alikuwa katika ibada bila ya kulala). Imam alihiji mara 55. Alihitimisha Quran Tukufu kila siku kimoja na usiku kimoja. Pia alikuwa akihitimisha Quran Tukufu katika rakaa moja ama mbili. Alikuwa mcha Mungu sana kiasi cha kufunga mwaka mzima (isipokuwa siku zile 5 zilizokatazwa) kwa muda wa miaka 30. Mahala alipofariki, alisoma Quran Tukufu 7,000.

WATUKUFU WAISLAMU TUPO JAMANI!!!

Mwezi Sha'abaan mwaka 150 Hijria, Imam aliiaga dunia hii huko Iraq akiwa katika hali ya sala, akiwa na umri wa miaka 70. Jeneza lake lilisaliwa mara 6 na kila mara waumini wapatao 50,000 walihudhuria na wengine walikuja kumuombea kwenye kaburi lake kwa siku karibu 20 hivi.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa.

 

JazakAllah.

Jan 25, 2025

Mi-iraj - PT 5 (MWISHO) [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo. Namalizia risala yetu kuhusu msafara wa Isra na Mi-'iraj. In sha Allah risala ya mwezi Sha-'abaan itafuata, kwani leo ni mwezi mosi Sha-'abaan. 

 

Baada ya kumshukuru Allah na kumtakia Rahma Mtume Muhammad , hapo juu ni aya ya 8 HADI 10 ya Sura Najmi, inayozungumzia Mtume Muhammad kuonana na Allah.

 

Mtume Muhammad alishuhudia Pepo na moto na baadae kufika Sidrah, ambapo alisikia sauti ya SUB-HANALLAH, ALHAMDULILLAH. Mtume Muhammad aliuliza ni kitu gani hiyo? Jibrail akajibu kuwa Sidrah, ambayo ni mti mkubwa, Malaika huleta dhikri. Hapo ndipo tamati ya Malaika. Mtume Muhammad alimwambia Jibrail waendelee lakini Jabirail akamjibu kuwa akisogea hatua moja kutoka hapa basi mbawa zake zitaungua kutokana na Nuru ya Allah; akamuambia Mtume Muhammad aendelee na safari.

Hapa ndipo Jibrail alimuomba idhini Mtume Muhammad ili amuonyeshe utukufu aliojaaliwa na Allah; kwani siku zote hizo Jibrail alikuwa akimjia Mtume Muhammad katika sura ya binadamu tu. Jibrail alipoondoa pazia mbawa zake 600 zikaonekana na ukubwa wa kila mbawa ulizidi hata ukubwa wa ardhi yote ya dunia. Wanazuoni wanasema lau kama Mtume Muhammad angemuonyesha utukufu wake, basi Jibrail angezimia pengine hadi kiyama.

Baada ya hapo Jibrail alimuomba Mtume Muhammad amtakie idhini kutoka kwa Allah kuwa siku ya kiyama wakati umma wake utakapopita kwenye njia nyepesi, basi yeye atande mbawa zake kuwasalimisha wapite kwa raha.

Baada ya hapo Mtume Muhammad alimpanda Rafraf na kuelekea juu zaidi. Baada ya kupita Arshi ndipo alimuona na Allah kwa macho yake, na hapo ndipo alimkaribia Allah. Kisha Allah Alimjaalia wahyi. Allah Alimuuliza je umeleta nini?

Mtume : Attahiyatu lillahi wasswalawaatu wattayyibaatu.

Allah : Assalaamu alaika ayyuhan Nabiyyu warahmatullahi wabarakaatuhu (salamu ziwe juu yako ewe Mtume pamoja na Rahma na Baraka).

Mtume : Assalaamu alaina wa-alaa ibadillahis swaalihin (salamu ziwe juu yetu na waja wako wema).

Hapo ndipo Allah Alimzawadia sala 50 za kutwa nzima. Mtume Muhammad alianza safari ya kurudi, lakini alipokutana na Mtume Musa katika mbingu ya 6, alimuambia arudi kwa Allah ili zipunguzwe kwani ummah wake walifaradhishiwa sala 2 tu kutwa nzima na walishindwa. Mtume Muhammad alirudi tena kwa Allah kutaka kupunguziwa, na Allah alimpunguzia sala 5. Alipofika tena kwa Mtume Musa, aliambiwa bado ni nyingi na kurudi tena kwa Allah. Kila nenda rudi sala 5 zinapungua hadi kusalia sala 5 na hapo ndipo Mtume Muhammad alisema sasa anaona haya kurudi tena kwa Allah. Ila Allah Alimuambia kuwa ummah wako itasali sala 5 tu lakini Sisi tutamjaalia thawabu za sala 50.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa.

 

JazakAllah.

Jan 23, 2025

Mi-iraj - PT 4 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo. Tunaendelea na risala yetu kuhusu msafara wa Isra na Mi-'iraj. 

 

Baada ya Kumshukuru Allah na kumtakia Rehma Mtume Muhammad , hapo juu ni aya ya kwanza ya Sura Bani Israil, ambayo inazungumzia msafara wa miraji.

 

Tafsiri ya aya:

Utukufu ni Wake Yeye Aliyempeleka Mja Wake katika sehemu tu ya usiku kutoka Msikiti wa Haraam (Makkah) hadi Msikiti wa Aqsa (Palestina), ambao umezungukwa na Baraka Zetu, ili Tumuonyeshe baadhi ya alama zetu. Hakika Allah ndiye Mwenye Kusikia Mwenye Kuona.

 

Mtume Muhammad alipoanza safari ya Masjidul Aqsa, njiani alimuona Mtume Musa akisali ndani ya kaburi lake. Hapa tunapata kufahamu kuwa Mitume si tu wapo hai ndani ya makaburi yao, bali huwa wanasali na pia hupata rizki.

 

Mtume Muhammad alipofika Masjidul Aqsa, Jibrail alitoboa sehemu moja iitwao Sakhra na kisha kumfunga mnyama wao. Kisha Jibrail alitoa adhana juu ya Msikiti wa Sakhra na kurudi Masjidul Aqsa. Hapa Mitume wote walikuwepo na kila mmoja akawa anafikiria je ni Mtume Adam ambae ni baba wa binadamu wote, ndiye atakaesalisha leo? Au Khalili wa Allah, Mtume Ibrahim? Au ni Mtume Nuh kwani baada ya tufani ya zama zake, masuala ya uzaaji ulianza kupitia yeye. Lakini Jibrail alimshika mkono Mtume Muhammad na kumpeleka mbele na kumuambia awa imamu wa Mitume wote. Baada ya sala, kila Mtume alisoma khutba ya kumsifu Mtume Muhammad .

 

Baada ya hapo Mtume Muhammad alifuatana na Jibrail kuelekea mbinguni. Kuna riwaya 2; (1) walienda kumtumia mnyama yule yule Buraaq au (2) Miraji ni jina la ngazi mmoja na hivyo walitumia ngazi hiyo kuelekea juu. Walipofika mbingu ya 1, mlango ulikuwa umefungwa. Jibrail alipiga hodi na kuulizwa ni nani? Alijibu mimi Jibrail niko na Mtume Muhammad . Baada ya kuulizwa kama Mtume Muhammad ameitwa, Jibrail akajibu kuwa ndiyo.

 

Mtume Muhammad alimuona mzee mmoja ambae kila akiangalia vivuli upande wake wa kulia basi hutabasamu lakini anapoangalia vivuli upande wa kushoto basi hulia. Mtume Muhammad aliuliza ni nani huyo na kwa nini mara hutabasamu na mara hulia? Jibrail alijibu kuwa msalimie huyu ni mtume Adam, upande wake wa kulia ni watoto wake walioleta imani na ndyo maana hutabasamu akiwaona. Wale wa kushoto ni watoto wake waliokataa imani na ndyo maana hulia akiwaona.

 

Mtume Muhammad alianza kuchupa mbingu moja baada ya nyingine huku akikutana na Mitume kila mbingu. Mbingu wa 2 alikutana na Mtume Yahya na isa, ya 3 Mtume Yusuf, ya 4 Mtume Idris, ya 5 Mtume Harun, ya 6 Mtume Musa nay a 7 alikutana na Mtume Ibrahim aliekaa kwa kuegemea Baitul Maamur. Baitul Maamur ni kibla ya Malaika mbingu ya 7, ambamo kila asubuhi na jioni Malaika 70,000 wapya huingia hapo. Mtume Muhammad aliwasalisha Malaika.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa.

 

JazakAllah.

Jan 22, 2025

Mi-iraj - PT 3 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

Natumai hamjambo. Leo ni usiku wa Isra wal Mi-'iraj.

Picha hapo chini ni sehemu takatifu mno ndani ya Masjidul Aqsa, nchini Palistina, ambapo Mtume alianza safari yake hapo ya kwenda mbinguni. Jiwe hilo linaitwa SAKHRAA.

Jan 21, 2025

Mi-iraj - PT 2 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo. Tunaendelea na risala yetu kuhusu msafara wa Isra na Mi-'iraj. Ijumaa Kareem

 

 

Kwanza kabisa hebu iangalie kwa makini jiwe katika picha niliyoambatanisha. Usiku wa Mi-'iraj wakati Mtume alipoanza safari ya kupaa mbinguni pamoja na mnyama Burraq, hilo jiwe nalo likaanza kupaa. Hapo ndipo Mtume alipoiamuru kusimama, na kwa kuwa ilikuwa imeshaanza kupaa basi jiwe ikasimama hivyo hivyo hewani na hadi leo hii jiwe hilo lipo kando kidogo na Masjidul Aqsa, Palestina.

 

 

 

 

 

Baada ya Kumshukuru Allah na kumtakia Rehma Mtume Muhammad , hapo juu ni aya ya kwanza ya Sura Bani Israil, ambayo inazungumzia msafara wa miraji.

 

Tafsiri ya aya:

Utukufu ni Wake Yeye Aliyempeleka Mja Wake katika sehemu tu ya usiku kutoka Msikiti wa Haraam (Makkah) hadi Msikiti wa Aqsa (Palestina), ambao umezungukwa na Baraka Zetu, ili Tumuonyeshe baadhi ya alama zetu. Hakika Allah ndiye Mwenye Kusikia Mwenye Kuona.

 

Imeelezwa kwenye vitabu vya Bukhari na Muslim kuhusiana na msafara huo kuwa Mtume Muhammad alikuwa nyumbani kwa Ummi Haani, kisha aliletwa sehemu inaitwa Hatim ndani ya Msikiti Mtukufu wa Makkah. Hapa alipasuliwa kifua, moyo ulitolewa na kuoshwa na maji matukufu ya zamzam na kujazwa hikma ndani yake na kisha kurudishwa na baada ya hapo kifua kikashonwa. Baada ya hapo Malaika mtukufu Jibrail Alaihissalaam alimuambia kuwa Allah Amemuita. Aliletwa mnyama mmoja aitwae Burraaq, ambae ni mkumbwa kuliko punda na mdogo kuliko farasi, aliye na kasi kiasi cha kuwa hatua yake moja umbali wake ni sawa na tamati ya sisi kuona. Mtume Muhammad alimpanda na kuanza safari ya kwenda Msikiti wa Aqsa.

 

Mtume Muhammad alionyeshwa baadhi ya alama wakati anaelekea Msikiti wa Aqsa, nazo ni kama ifuatavyo:

 

1. Mtume Muhammad aliwaona baadhi ya watu wakilima, huku wanaendelea kupanda mbegu na papo hapo mazao yalikamilika na watu hao kuvuna na kupata faida. Mtume Muhammad alifahamu kila kitu, lakini kuuliza kwake ni kwa ajili ya mafundisho kwetu.

Aliuliza: hivi ni kina nani hao?

Jibrail alimjibu: hawa ni katika ummah wako wanaotoa katika njia ya Allah; mfano kujenga Misikiti, madrasa, nk basi hupata faida papo hapo tu.

 

2. Mtume Muhammad aliwaona watu wamelala na vichwa vyao kupondwa, kisha husima wakiwa wazima na baadae hulala na vichwa hupondwa.

Aliuliza: ni kina nani hao:

Jibrail almijibu: hao ni wale wanaopendelea kulala wakati wa sala ya Alfajiri, wanaona usingizi mtamu na pia huacha sala. Wataadhibiwa hivyo hadi siku ya Kiyama.

 

3. Mtume Muhammad aliwaona baadhi ya watu wakila mawe na miti porini lakini hawashibi.

Aliuliza: ni kina nani hao?

Jibrail alimjibu: hao ni wale wasiotoa zaka kutokana na walichojaaliwa na Allah na pia hula haki za masikini.

Mtume Muhammad amesema kuwa toeni zaka ili mkinge mali zenu.

 

4. Mtume Muhammad aliwaona watu ambao wamewekewa vyakula mbalimbali halali na vizuri sana mbele yao, lakini wanayaacha hayo na kukimbilia kula vyakula vibaya vilivyooza na kutoa herufu mbaya.

Aliuliza: ni kina nani hao?

Jibrail alimjibu: hao ni wale wanaowaacha wake zao halali na hukimbilia kwa wanawake wa nje na kutenda mambo ya haramu.

 

5. Mtume Muhammad alimuona mtu mmoja mwembamba sana aliyekusanya kuni nyingi. Alipotaka kuubeba akashindwa. Badala ya kupunguza kuni kidogo, akaenda porini kuongeza kuni zingine.

Aliuliza: ni nani huyo?

Jibrail alimjibu: ni yule mwenye kuleta khiyana kwenye amana za watu na pia huweka tamaa apewe amana zaidi.

 

6. Mtume Muhammad aliwaona baadhi ya watu wakikata taya zao kwa kisu kikali. Wanapomaliza za upande wa kulia na kukata za upande wa kushoto, za kulia huwa sawa.

Aliuliza: ni kina nani hao?

Jibrail alimjibu: hao ni wale wanaoeneza fitina kwa ulimi wao.

 

Hizo ni baadhi alama alizoonyeshwa Mtume Muhammad katika msafara wake.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa.

 

JazakAllah.

Jan 20, 2025

Mi-iraj - PT 1

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo. Kama mnavyofahamu kuwa mwezi tulionao ni wa Rajab na usiku wa Jumatatu (24/4/2017) kuamkia Jumanne (25/4/2017) ni katika usiku takatifu katika historia ya Kiislam, kwani ni usiku ambamo Mtume wetu mpendwa alijaaliwa muujiza wa isra na Mi-'iraj.

Hivyo nitakuwa natuma risala fupi fupi kuhusu msafara huo in sha Allah.

 

 

 

 

Baada ya Kumshukuru Allah na kumtakia Rehma Mtume Muhammad Swall-Allahu Alaihi Wasallam, hapo juu ni aya ya kwanza ya Sura Bani Israil, ambayo inazungumzia msafara wa miraji.

 

Ieleweke kuwa kila Mtume aliyeletwa hapa duniani alipewa muujiza au miujiza.

Lakini Mtume Muhammad Swall-Allahu Alaihi Wasallam aliletwa kama muujiza licha ya kupewa miujiza mingi, mmojawapo ukiwa huu msafara wa miraji.

 

Tafsiri ya aya:

Utukufu ni Wake Yeye Aliyempeleka Mja Wake katika sehemu tu ya usiku kutoka Msikiti wa Haraam (Makkah) hadi Msikiti wa Aqsa (Palestina), ambao umezungukwa na Baraka Zetu, ili Tumuonyeshe baadhi ya alama zetu. Hakika Allah ndiye Mwenye Kusikia Mwenye Kuona.

 

Tukiichunguza aya peke yake tu ina nukta nyingi za kuzingatia.

1. Kwanza kabisa, Allah Ametaja Utukufu Wake kwa kuanza aya. Hii ni kuukata kata kabisa utata uliotokea na utakaotokea kwani mwenye kuleta utata katika msafara huu, basi moja kwa moja analeta mashaka katika uwezo wa Sub-hana!

2. Baadhi ya watu wanadai kuwa eti Mtume Swall-Allahu Alaihi Wasallam alioteshwa tu kwenda mbinguni na si kuwa alienda (yaani eti mwili wake haukuenda)!!! Sehemu ya pili ya aya inafafanua : "ALIYEMPELEKA MJA WAKE". Sehemu ya aya haisemi kuwa "alimuotesha"! Hivyo mwenye kupinga msafara huo wa kiwiliwili na roho basi atatoka katika Uislamu.

3. Msafara huu ulifanyika katika sehemu fupi mno ya usiku. Riwaya moja inaelezea ufupi wa msafara kuwa maji aliyotawadhia Mtume Swall-Allahu Alaihi Wasallam yalikuwa bado yanasambaa ardhini wakati Mtume Swall-Allahu Alaihi Wasallam aliporejea. Riwaya nyingine inasema kuwa Mtume Swall-Allahu Alaihi Wasallam alipofungua mlango kutoka chumbani mwake, ile komeo (cheni) bado ilikuwa ikicheza aliporejea! Kwa ufupi hatuwezi kupata picha ya ufupi wa msafara huo na ndiyo maana ikatajwa kuwa ni muujiza.

4. Vile vile ni sababu ya msafara kuwa usiku tu? Sababu kuwa iliyotajwa kuwa ili watu wasipate kuona. Imani ni kuamini kisichoonekana, hivyo lau kama msafara ungetokea mchana basi wengi wangemuona Mtume Swall-Allahu Alaihi Wasallam akienda na hivyo kupima imani ingekuwa ngumu.

5. Kwa nini sehemu ya kwanza ya msafara ulikuwa kutoka Makkah hadi Palestina? Hii ni kwa sababu Waarabu walikuwa na misafara ya mara kwa mara baina ya sehemu hizo. Hivyo kuwafahamisha kuwa msafara huu wa Mtume Swall-Allahu Alaihi Wasallam baina ya sehemu hizo katika muda mfupi ili wawe na picha ya sehemu wanazoambiwa.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa.

 

JazakAllah.

Jan 5, 2025

RAJAB-UL-MURAJJAB - PT 4 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo. Mwezi 6 Rajab mmoja katika kiongozi wa masharifu kwa tarika ya Chishti aliiaga dunia na ifuatayo ni risala fupi.

 

 

SULTAN MUINUDDIN CHISHTI RAHIMAHULLAH.

 

Sultan Muinuddin Chishti Rahimahullah alizaliwa Khorasan, Afghanistan. Alikuwa mwaka sambamba na Sayyid AbdulQadir Jilani Qaddasallahu Sirrah. Kwa kuwa Sayyid AbdulQadir Jilani Qaddasallahu Sirrah alishachaguliwa kuiongoza bara la Uarabuni kuhuisha dini, Mtume alimchagua Sultan Muinuddin Chishti Rahimahullah kuiongoza bara Hindi katika kuinusuru dini. Hakuwahi kupita maeneo ya bara Hindi wala hakufahamu kabisa lugha ya kihindi. Mtume alimjia kwenye ndoto na kumuonyesha njia ya kwenda bara Hindi na kisha alimtemea mate matukufu na hivyo akafahamu lugha ya kihindi kwa fasaha.

 

Kutokana na karama zake, wachawi wa kibaniani wakajua huo ni uchawi, hivyo mfalme wa huko aliwakusanya wachawi wakubwa kukabiliana nae lakini wote walishindwa na hatimaye kusilimu. Zaidi ya mabaniani milioni 9 walisilimu kutokana na karama zake tofauti. Hatimaye aliiaga dunia mwezi 6 Rajab.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa

 

JazakAllah.

Jan 3, 2025

RAJAB-UL-MURAJJAB - PT 3 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo. Mwezi 4 Rajab ambamo mmoja katika maimamu wetu wane, Imam Shafi-'I aliiaga dunia.

 

 

Baada ya kumshukuru Allah na kumtakia Rahma Mtume Muhammad , aya hapo juu ya 36 ya Sura Tawbah, inazungumzia utukufu wa miezi minne. Mwezi Rajab, ambao ni mmojawapo kati ya miezi hiyo minne, mwezi ambao una fadhila tele. Ni mwezi ambamo dua hukubalika.

TAFSIRI: Bila shaka idadi ya miezi kwa Allah ni miezi kumi na mbili katika kitabu cha Allah tangu Alipoumba mbingu na ardhi, miongoni mwao minne ni yenye huruma (tukufu). Hii ni dini iliyonyooka na hivyo msidhulumu nafsi zenu katika miezi hizo. Na piganeni na washirikina wote kama wao wanavyopigana nanyi nyote, na jueni kuwa Allah yu pamoja na wachamungu.

 

IMAM SHAFI-'I RAHIMAHULLAH.

Jina la Imam Shafi-'I ni Muhammad bin Idris bin Abbas bin Uthman bin Shafi-'I bin Saib bin Ubeid bin Abdi Yazid bin Hashim bin Abdul Muttalib bin Abdi Manaf.

 

Abdi Manaf ni katika ukoo wa nne wa Mababu zake Mtume . Ukoo wa Mtume Swall-Allahu Alaihi Wasallam uko hivi: (Sayyidina) Muhammad bin Abdullah bin Abdul Muttalib bin Hashim bin Abdi Manaf. Hivyo Mtume amezaliwa kupitia mwanae Abdi Manaf (Hashim) wakati Imam Shafi-'I amezaliwa kupitia Abdul Muttalib.

Imam Shafi-'I amekuwa maarufu kwa jina hilo (Shafi-'i)  kupitia kwa babu yake katika ukoo wa tatu (Shafi-'i).

 

Wazazi wake wanatokana na kabila maarufu la kiarabu la Bani Hashim. Baadhi ya sababu ya yeye kuwa na kipaji hicho ni kuwa alikuwa : Imam (kiongozi – wa Dini), Mwanasheria (wa masuala ya sharia za Dini), Mcha Mungu na mtu mwenye hekima na busara. Alikuwa mwandishi wa vitabu vikubwa 14 vya kanuni na falsafa vya sharia ya Kiislam na pia vitabu vingine vidogo zaidi ya 100.

 

Kila alipopatwa na tatizo, Imam Shaifi-'I alielekea Baghdad kudhuru kaburi la Imam Abu Hanifa, kisha husali rakaa 2 na kumuomba Allah kupitia (wasila) kwa Imam Abu Hanifa. Imam Shafi-'I mwenyewe amesema kuwa hakika maombi yanakubalika katika kaburi la Imam Abu Hanifa.

 

Imam Shafi-'I alikuwa mwanafunzi wa Imam Malik Radwiy-Allahu Anhu. Alikuwa akihitimisha Quran (Msahafu) nzima katika usiki moja tu mwezi Ramadhani. Alihifadhi Qurani nzima akiwa na umri wa miaka 7 tu.

 

Alizaliwa mwaka 150 Hijriya (mwaka ambamo Imam Abu Hanifa aliiaga dunia), huko Asqalan au Mina au Ghizza. Aliishi Makkah na aliiaga dunia hii akiwa na umri wa miaka 53, mwaka 204 Hijriya huko Misri.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa

 

JazakAllah.

Jan 1, 2025

RAJAB-UL-MURAJJAB - PT 2 [Kiswahili]

Assalaamu alaikum,

 

Natumai hamjambo. Mwezi wa Rajab tumeshauanza na ifuatayo ni sehemu ya kwanza ya risala …

 

 

Baada ya kumshukuru Allah na kumtakia Rahma Mtume Muhammad , aya hapo juu ya 36 ya Sura Tawbah, inazungumzia utukufu wa miezi minne. Mwezi Rajab, ambao ni mmojawapo kati ya miezi hiyo minne, mwezi ambao una fadhila tele. Ni mwezi ambamo dua hukubalika.

TAFSIRI: Bila shaka idadi ya miezi kwa Allah ni miezi kumi na mbili katika kitabu cha Allah tangu Alipoumba mbingu na ardhi, miongoni mwao minne ni yenye huruma (tukufu). Hii ni dini iliyonyooka na hivyo msidhulumu nafsi zenu katika miezi hizo. Na piganeni na washirikina wote kama wao wanavyopigana nanyi nyote, na jueni kuwa Allah yu pamoja na wachamungu.

                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                   

Mwezi wa saba katika kalenda ya Kiislam inaitwa RAJAB, ambayo inatokana na neno "TARJIB", yenye maana ya heshima na hata zama za ujahili Waarabu waliuheshimu sana mwezi huu kwa kuacha mapigano na mauaji, wakisema ni mwezi wa Mwenyezi Mungu.

Mtume amesema kuwa Rajab ni mwezi wa Allah, Shaaban ni wa kwangu na Ramadhani ni ya ummah wangu.

 

Mtume amesema kuwa Rajab ni mwezi wenye fadhila nyingi, thawabu ya amali njema huwa maradufu ya thawabu ya kawaida. Mwenye kufunga swaum 1 ndani ya Rajab, basi ni sawa na kufunga mwaka mzima.

Siku 1 Mtume Isa Alaihissalaam alipokuwa akipita karibu na mlima mmoja, aliona nuru sehemu Fulani ya mlima. Alimuomba idhini Allah ili aweze kuzungumza na mlima. Mlima ilimuuliza nini atakacho?  Mlima ikasema kuwa ndani yake kuna Mcha Mungu mmoja nan i kwa sababu ya huyo mlima una nuru. Mtume Isa Alaihissalaam alimuomba Allah aonyeshwe huyo mtu na mara mlima ikapasuka na akaonekana Mcha Mungu aliye mzuri sana. Alisema kuwa yeye ni katika watu wa Mtume Musa Alaihissalaam na alimuomba Allah Amjaalie maisha marefu ili aweze kushuhudia zama za Mtume wa mwisho Muhammad na hivyo ahesabiwe miongoni mwa ummah wa Mtume wa mwisho. Mcha Mungu huyo alikuwa mlamani humo kwa miaka 600. Kisha Mtume Isa alimuuliza Allah kama kuna Mcha Mungu ardhini zaidi ya huyo bwana? Allah alimjibu: "Ewe Isa, lau kama mja wangu katika ummah wa Mtume wa mwisho akifunga siku moja tu ya mwezi Rajab, basi huyo mja kwangu atakuwa Mcha Mungu zaidi kuliko huyo bwana!! (SUB-HANALLAH).

 

Baadhi ya tarehe muhimu:

Tarehe 1 – Mtume Nuh Alaihissalaam alianza safari na wafuasi wake katika mashua (meli) waliyoitengeneza.

Tarehe 4 – Vita vya Safin

Tarehe 4 – Imam Shafi-I Rahmatullahi Alaihi kuiaga dunia

Tarehe 6 – Sayyidina Moinuddin Chishti (kiongozi wa Walii kwa twariqa ya Chishtiya) kuiaga dunia

Tarehe 27 – Msafara wa isra na Mi-iraj ya Mtume .

 

 

 

Tarehe 1 Mtume Nuh na wafuasi wake walianza safari katika meli kabla ya tufani kali iliyowaangamiza waliompinga.

 

 

Tarehe 4: Imam Shafi aliaga dunia. Jina lake ni Muhammad bin Idris na kizazi chake cha 4 kinakutana na kile cha Mtume Muhammad kwa Abdi Manaf. Amezaliwa mwaka 150 hijria na kufariki mwaka 204h mjini Cairo, Misri. Alikuwa akikhitimisha msahafu mmoja kila siku katika mwezi Ramadhani. Kila alipopatwa tatizo, basi huenda kuizuru kaburi la Imam Abu Hanifa na kisha huomba dua akimtawassul.

 

 

 

Tarehe 6: Walii mkubwa wa Allah Moinuddin Chishti aliaga dunia nchini India. Walii huyo alikuwa mwaka sambamba na Sheikh Abdul Qadir Jilani Qaddasallahu Sirrah. Mtume Muhammad alimjaalia uwalii wa bara hindi. Mabaniani milioni 9 walisilimu kwa jitihada zake.

 

 

Tarehe 27: Msafara wa Isra na miraj ya Mtume Muhammad ambayo insha Allah tutaanza kuizungumzia hapo baadae.

 

Maswali / maoni yanakaribishwa

 

JazakAllah.

 

Visitor's Traces

1,278 Pageviews
Mar. 07th - Apr. 07th

Total Page views

764951