Ads 468x60px

Jan 9, 2014

MAULIDI - PT 1‏ (Kiswahili)



Natumai hamjambo na mpo katika maandalizi ya shamra shamra za Maulidi (mazazi ya Mtume SwallAllahu Alaihi Wasallam.
In sha Allah nitakuwa nikituma risala kuhusiana na sifa za Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam kama ilivyo ndani ya Quran na Hadithi na pia masuala ya wapingao Maulidi.
Eleweni ya kuwa siku ya Maulidi kwa mwaka huu ni Jumanne 14/1/2014, ina maana itasomwa Jumatatu usiku. Kwa kuwa mwezi huu unaitwa RABI-UL-AWWAL (Mfungo 6), RABI’ maana yake ni furaha, hivyo ninamuomba kila mmoja wetu ajitahidi kusoma Maulidi nyumbani kwake hata kama na familia yake tu, walau mara moja katika mwezi huu; in sha Allah itamletea faida kubwa.
 
Baada ya kumshukuru Allah na kumtakia Rahma Mtume Muhammad Swallallahu Alaihi wasallam, aya hapo juu ya 15 kutoka Sura Al Maidah (15), inayozungumzia kuletwa kwa Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam.
TAFISIRI: Enyi watu wa Kitabu! Amekujieni Mtume wetu anaekufichulieni mengi mliyokuwa mkiyaficha katika kitabu na anaesamehe mengi. Bila shaka imekujieni kutoka kwa Allah Nuru na Kitabu kinachobainisha.

Allah Azza waJallah amesema: “Hakika imekuja kwenu Nuru” (Quran 5:15). Vivyo hivyo kuna aya nyingi za Quran Tukufu zinazoelezea kuja kwa Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam hapa duniani. Mmojawapo ya aya inasema: “Hatukupeleka wewe ila uwe ni Rahma kwa walimwengu” (Quran 21:107), pia “Hakika imekuja kwenu Nuru na uthibitisho iliyowazi” (Quran 5:15), pia “Hakika amekuja Mtume miongoni mwenu” (Quran 9:128) na pia “Allah Ana Hisani juu ya Waumini kwa kumleta Mtume miongoni mwao” (Quran 3:164). Vile vile kuna aya nyingi za namna hii na hata kwenye Hadithi imeelezwa kuja kwa Mtume.
Kuelezea kuja kwa Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam, imetajwa kama: “Ewe Habibi Nimekutuma …”, “Mtume amekuja …” na “ameletwa …”.Mmoja akichunguza kwa makini maneno haya, ataamini kabisa kuwa mtu analetwa au kupelekwa ni yule alikuwepo sehemu moja mwanzoni. Hivyo itabidi tukubali kuwa Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam – Roho ya ulimwengu, tumaini la shida, Masiha kwa watu, Rahma kwa walimwengu – alikuwa sehemu fulani kabla ya kuletwa hapa duniani. Kabla ya kuletwa Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam, hali ya dunia haikuwa nzuri. Kila kitu kilikuwa katika mchafuko. Ukafiri ulikuwa umeenea kila sehemu. Ulevi, kamari, riba na rushwa ilikuwa ni jambo la kawaida. Mitaani zinaa, ndoa ya jinsia moja, husuda, kusengenya, uadui na chuki zilienea. Ufidhuli, unyang’anyi na uuaji ilikuwa ndiyo maisha ya kila siku. Hapakuwepo hata herufu ya upendo, heshima na unyenyekevu miongoni mwa watu. Pia hapakuwepo na hifadhi ya maisha na mali. Jumuiya iliharibika sana kiasi cha mzazi kumzika hai binti wake. Katika wakati wa uharibifu kama huo, tumaini kwa wadhaifu, Rahma kutoka kwa Allah, Mtume wetu Mpendwa Swallallahu Alaihi Wasallam alizaliwa alfajiri ya Jumatatu, mwezi 12 Mfungo 6 (Rabi-ul-Awwal). Siku ya kuzaliwa Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam, ulimwengu mzima uliingia mwangaza, ukafiri ulianza kuvurugika, moto wa uajemi ulizimika, upepo wa imani ulianza kuvuma, bendera yaTauhid ili pandishwa, Nuru ilianza kuenea na wengi walioabudu miungu 360 (sanamu) sasa waligeuka katika ibada ya Allah Mmoja.
Kuna kila sababu ya Muislamu kuadhimisha siku hiyo Tukufu. Isitoshe Kiyam ya kumsalia Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam wakati Alfajiri inapoingia mwezi 12 (muda wa kuzaliwa Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam) na kisha dua inayoombwa muda huo, inakubalika moja kwa moja. Hivyo ni bora kusoma Qasida Burdai (YA RABBIBIL MUSTAFA BALLIGH MAQAASWIDANA …) usiku huo ili kupata faida kwani ni Qasida iliyokubalika mbele ya Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam.
Ni uthibitisho wa Hadith-ul-Qudsi, Allah Amesema: “Lau kama nisingemuumba Muhammad Swallallahu Alaihi Wasallam, basi nisingeumba Pepo, moto, Mwezi, Jua, mbingu na ardhi, usiku na mchana na Mitume na Malaika”. Si hivyo tu bali Allah amesema kuwa “E Mpendwa! Lau kama nisingekuumba wewe basi Nisingejidhihirisha”.
Nuru ya Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam iliumbwa kabla ya chochote, kama alivyosema: “Kitu cha kwanza Allah alichokiumba ni NuruYangu”. Nuru hii ya Mtume Swallallahu Alaihi Wasallam ilikuwa juu zaidi karibu na Muumba wake kwa miaka 4,000. Allah alipokusudia kuumba, Aligawanya Nuru hii katika sehemu 4.
1) Aliumba Kalamu
2) Meza Tukufu
3) Arshi
4) Viumbe vilivyosalia

Maswali / maoni yanakaribishwa.
JazakAllah,
Muhammad KHATRI 

0 comments:

Post a Comment

Enter your Comment here...

 

Visitor's Traces

Total Page views