Ads 468x60px

Sep 13, 2013

MTUME IBRAHIM - PT 3‏ (KISWAHILI)


Assalaamu alaikum,
Natumai hamjambo. Ijumaa Kareem 
Tunaendelea na risala juu ya maisha ya Mtume Ibrahim Alaihissalaam.
AYA:  ALAMTARA ILALLADHI HAAJJA IBRAHIMA FI RABBIHI AN AATAHULLAHUL MULK.
Baada ya kumshukuru Allah na kumtakia Rahma Mtume Muhammad Swallallahu Alaihi wasallam, imesomwa kipande cha aya 258 ya Sura Baqara, inayozungumzia Mtume Ibrahim Alaihissalaam.
Siku moja watu wote walienda kwenye sherehe nje ya mji. Walitaka Mtume Ibrahim aende nao lakini alisema “INNI SAKIM” – mimi mgonjwa. Wote walipoondoka, Mtume Ibrahim aliingia chumbani mwao na kuvunja masanamu yote na kisha kuacha nyundo kwenye bega la sanamu mkubwa ili aweze kujenga hoja ya Kumpwekesha Allah mbele yao.
Watu wote waliporudi jioni na asubuhi yake kuingia chumbani kuabudu, walikuta miungu yao imevunjwa. Taarifa zikamfikia mfalme kuwa inawezekana ni kazi ya yule kijana wa Azar ambae huzungumzia mabaya ya miungu yao. Mtume Ibrahim aliitwa kwa mfalme kujibu tuhuma hizo.
Mfalme: Tueleze ni kazi ya nani hiyo?
Ibrahim: Mnaniuliza mimi? Ingekuwa mkawauliza wenyewe hivi ni nani aliyewapiga, mimi naona ni kazi ya hili sanamu kubwa kwani ndiye aliyeshika nyundo.
Walitamka kile ambacho Mtume Ibrahim alikusudia wao kusema, kuwa “sisi tuwaulize nini hao? Hawawezi kuzungumza wala kutembea wala kujizuia kitu, watajibu nini hao?
Ibrahim: Mnashangaza sana kuwaamini miungu wasio na uwezo wa kuwasaidia? 
Wanazuoni wanasema kuna riwaya 3 inayoelezea kutokea kwa mjadala huo.
1)    Hapa Namrudi alipokuwa hana la kusema ndipo mjadala ukaanza.
2)    Mjadala ulitokea kabla Mtume Ibrahim kuingizwa kwenye moto.
3)   Mwaka mmoja ulitokea ukame na Namrudi ndiye aliyekuwa akigawa chakula. Mtume Ibrahim alipofika kwa Namrudi, aliambiwa amsujudie. Mtume Ibrahim alimwambia kuwa yeye anamsujudia Mola wake tu. Namrudi alimuuliza kuwa nani Mola wake? Mtume Ibrahim akamwambia Mola wake ni mwenye kuhuisha na kufisha. Namdrudi akawatoa wafungwa wake wawili, kamwachia huru mmoja na kamuua mwingine; kisha kasema hata mimi nahuisha na kufisha.
Hapa Namrudi hakuweza kuelewa maana halisi ya kuhuisha na kufisha. Allah kaumba binadamu kutokana na tone tu la maji, kisha binadamu huyo anakufa na kuwa udongo na siku ya Kiyama Allah Atamfufua binadamu huyo.
 Siku moja Mtume Ibrahim alimwomba Allah amuonyeshe jinsi Atakavyo huisha na kufisha ili moyo wake utulie. Allah Alimuambia awaite ndege wanne kisha awachinje na vichwa vyao kutupa kwenye mlima. Kisha achanganye nyama yao na kuweka kwenye bakuli moja. Sasa Ibrahim akaambiwa kuwaita wale ndege kwa majina yao na kichwa kinatoka mlimani  hadi kuchukua nyama yake na hupaa angani.
Mtume Ibrahim baada ya kuona ujinga wa Namrudi, ndipo alimwambia: Mola wangu huchomoza jua Mashariki, wewe ichomoze magharibi; ndipo Namrudi hakuwa na jibu na akaamuru Mtume Ibrahim aingizwe kwenye moto.
 Wanazuoni wanasema kuwa Namrudi hakuwa na la kusema, ila kama angepatwa na wazo la kumwambia Mtume Ibrahim kuwa “mimi nimeshindwa, ila mwambie Mola wako achomoze jua magharibi”. Basi Allah Alimjaalia Mtume Ibrahim kuwa angeashiria sehemu yoyote ya mbinguni, basi jua ingechomoza kutoka hapo, ili tu uongo wa Namrudi idhihirike.
Namrudi alikuwa na kiburi sana kiasi cha kwamba Malaika walimjia mara 3 kumkumbusha kuhusu imani na mara zote 3 aliwadharau.

Maswali / maoni yanakaribishwa
JazakAllah, 
Muhammad KHATRI 


0 comments:

Post a Comment

Enter your Comment here...

 

Visitor's Traces

Total Page views